Tuesday, November 29, 2016

MSANII WA WIKI - LEMBO JR

LEO KATIKA MSANII WA WIKI - EMMANUEL LEMBO JR

Rejoice Blog: Labda tuanze kwa kujua majina yako kamili na ikiwa unatumia jina tofauti kwenye kazi zako za muziki?

Lembo Jr: Jina langu ni Emmanuel Stephen Lembo, ila katika huduma nafahamika kama Lembo Junior
Lembo Jr

Rejoice Blog: Je, umeokoka? Unaabudu katika kanisa gani?

Lembo Jr: Nimeokoka nampenda Yesu, kwa sasa naabudu NAIYOTH CHURCH - GEITA

Rejoice Blog: Historia yako kwa kifupi ya kuimba, yaani ulianzaje na wapi ulianzia?

Lembo Jr: Naweza sema,nilianzia utotoni sundayschool kids choir...ila kuingia rasmi kwenye tasnia hii mpaka kuanza kusikika kwa medias ni 2007-2008 nikiwa UDOM

Rejoice Blog: Katika kuimba kwako, je, umeshatoa album yoyote? Majina ya albamu?

Lembo Jr: Mpaka sasa niko na 4 albums ila tatu ndizo zajulikana 1.TUTEMBELEE. 2 USIFIE JANGWANI. 3.UWE KILA KITU. 4.WINGU LIMESIMAMA WAPI

Rejoice Blog: Wimbo unaoupenda zaidi kati ya nyimbo zako ni upi?

Lembo Jr: mmmmmmh ni almost nyimbo zote nazipenda maana kila wimbo najua Mungu alinipaje ILA UWE KILA KITU, TUTEMBELEE NA USIFIE JANGWANI ni zaidi

Lembo Jr
Rejoice Blog: Ni kwa sababu gani unaupenda wimbo huo zaidi?

Lembo Jr: Nyimbo zina ushuhuda mkubwa sana sikuzipewa hivi hivi, nilipitishwa sana sanaaaaa

Rejoice Blog: Nani anasambaza na kusimamia kazi zako? Na je, anakusaidia vizuri?

Lembo Jr: Kwa sasa niko na Madam Gisela Malisa, yuko vyema

Rejoice Blog: Ni msanii gani wa muziki wa Injili anayekuvutia na unapenda kufuatilia kazi zake?

Lembo Jr: Sipho Makhabane, Emmanuel Mgogo

Rejoice Blog: Kuna mafanikio gani umeyapata katika kuimba nyimbo za Injili?

Lembo Jr: Yako mengi sana kiroho na kimwili. Kiroho; nimekua nikipokea shuhuda nyingi sana namna nyimbo zangu zimeokoa, zimeponya na kuganga NAFSI zilizokia zimejeruhiwa.  Kimwili kuna kupata kipato ingawa si kikubwa, ila MUNGU ni mwema. Na pia nimepata EXPOSURE kubwa sana ndani na nje ya mipaka ya Afrika
Lembo Jr

Rejoice Blog: Umekutana na changamoto gani katika huduma yako ya uimbaji?

Lembo Jr: Changamoto ni nyingi sanaaaa kiroho na kimwili pia kimwili zaidi ni PESA, nitatizo kikubwa, kiroho vita ni KUBWA sana

Rejoice Blog: Unaonaje muziki wa Injili hapa Tanzania? Na hasa wa aina unayoimba wewe?

Lembo Jr: Muziki huu naona kwa upande wangu uko vyema maana haujaniangusha

Rejoice Blog: Unatoa ujumbe gani kwa waimbaji wa nyimbo za Injili ambao kwa njia moja ama nyingine wanajisahau na kujichanganya na mambo ya dunia hii?

Lembo Jr: Kikubwa ni kurudi kwenye kusudi la MUNGU na kulitumikia Shauri la Bwana

Rejoice Blog: Zaidi ya kuimba ni kitu gani kingine unakifanya?

Lembo Jr: Kitaaluma nina Bachelor Degree ya Public Administration (Shahada ya Sanaa katika Utawala wa Umma), ingawa sijaajiriwa, ninafanya biashara zangu ndogo ndogo

Rejoice Blog: Je, kimaisha uko wapi? Ndoa na watoto vipi?

Lembo Jr: Naishi na familia yangu Geita, niko na mtoto mmoja tu

Rejoice Blog: Una ujumbe gani kwa Waimbaji wa Nyimbo za Injili hapa Tanzania?

Lembo Jr: Ujumbe TUIFANYE KAZI YA MUNGU KWA UNYENYEKEVU MKUU SANA

Rejoice Blog: Na kwa jamii inayoguswa na kuburudishwa na nyimbo za Injili una ujumbe gani kwao?

Lembo Jr: Waendelee kutusapoti kwa hali, mali na maombi.

Rejoice Blog: Ahsante sana Lembo Jr kwa muda wako, Mungu akubariki na kukuinua unavyoendelea kumtumikia kwa uaminifu

Lembo Jr: Nami NIWASHUKURU SANA SANA KWA MUDA WENU NA KUJALI KWENU MUNGU AWABARIKI SANAAAA

Huyo ndiye Emmanuel Stephen Lembo a.k.a Lembo Junior ambaye umepata kumfahamu zaidi kupitia Msanii wetu wa Wiki. Ukitaka kuendelea kufuatilia habari zake na kazi yake ya huduma, mpate kwa njia zifuatazo:

Emmanuel Lembo Jr:
Instagram: @lembojr
Facebook: Lembo Jr Emmanuel

~~~ UMEBARIKIWA! ~~~


Monday, November 28, 2016

MAOMBI YA KUFUNGUA MALANGO NA MILANGO - SEHEMU YA 3

Na Mchungaji Florian Katunzi - EAGT City Center

Wiki jana nilikufundisha juu ya aina za funguo za kufungua malango na milango, ambapo nilikwambia zipo aina tano na nikakufundisha funguo mbili kati ya hizo. Funguo ya kwanza ilikuwa ni Neno la Mungu na ya pili ilikuwa ni Imani.

Nilikwambia ya kuwa neno la Mungu ni kauli ya Mungu yenye Mamlaka, Uweza na Nguvu za ki-Mungu zenye kuleta mageuzi ya kiroho na kimwili. Pia nilikuonesha maandiko ambayo yanathibitisha hilo.

Katika kipengele cha imani ambacho ndicho tunachoendela nacho siku ya leo, nilikufundisha maana halisi ya imani na nilisema  Imani ni tendo la utii katika kuitikia kile Mungu alichokisema katika Neno lake.

Nilizama zaidi  na kukuonesha msingi wa kuwa na imani kwa Mungu ambao uko katika kweli tatu zilizobebwa na maana halisi ya Asili ya Mungu wetu. Kweli hizo ni  Hawezi Kubadilika, Hawezi Kushindwa na Hawezi Kudanganywa.

Endelea……….

Malango na Milango ni sharti ifunguliwe kwa Imani; sawasawa na Neno la Mungu. Kwa Imani tunalegeza viuno vya wafalme, Kwa Imani tunalegeza mafungo na vifungo vilivyowafunga watu wa Mungu. Kwa Imani tunafungua Malango na Milango iliyofungwa mbele yetu.

 “Tena itakuwa katika siku hiyo mzigo wake utaondoka begani mwako, na nira yake shingoni mwako, nayo nira itaharibiwa, kwa sababu ya kutiwa mafuta.” Isaya 10:27

Kila mzigo uliotwishwa katika nafsi yako unaondolewa begani mwako maana uwezo wake Kristo Yesu sasa umedhihirishwa ili kazi zote za yule mwovu shetani zivunjwe ndani mwa imani.

“Kwa maana vinyago vimenena maneno ya ubatili, nao waaguzi wameona uongo, nao wameleta habari za ndoto za uongo, wafariji bure; kwa sababu hiyo waenda zao kama kondoo, wateswa, kwa sababu hapana mchungaji.” Zekaria 10:2

Imani ni Ufunguo wa kufungua Malango na  Milango, tunaona Senakeribu analeta majeshi yake akiwa ameazimia kupiga watu wa Mungu na kuwatawala. Mfalme Hezekia  akasema na watu wake ili apate wakuwajenga Kiimani.

 “Iweni hodari, na wa moyo mkuu, msiogope, wala msifadhaike kwa sababu ya mfalme wa Ashuru, wala kwa majeshi yote walio pamoja naye; kwa maana yupo mkuu pamoja nasi kuliko aliye pamoja naye, kwake upo mkono wa mwili, ila kwetu yupo BWANA, Mungu wetu, kutusaidia, na kutupigania mapigano yetu. Na watu wakayategemea maneno ya Hezekia mfalme wa Ashuru.” 2Mambo ya Nyakati 32:7-8

Adui anakuja na neno lenye kuogofya ili kuifisha Imani yako, Senekarabu anatuma watu wenye kuhubiri hofu kwa kueleza historia ya Hezekia ya udhaifu.
Senekerebu anatuma watu wake wageuze neno la Mfalme Hezekia ili apate kuifisha Imani yao apate kuwapiga. Hezekia anataka kuonyesha waziwazi tofauti kati ya mkono wa mfalme wa Ashuru na mkono wa BWANA.

Nasi kanisa lazima tutambue ya kuwa kwetu upo mkono wa BWANA wenye nguvu ya Kuokoa na Kuponya hivyo lazima tusimame kwa Imani ndipo tupate kufungua Malango na Milango iliyofungwa mbele zetu, Maana pasipo IMANI haiwezekani kumpendeza Mungu. Kwa imani yote yanawezekana katika Kristo.

Imani ni chanzo kikuu cha kupokea kutoka kwa Mungu maana hakuna neno lolote lililo gumu la kumshinda Mungu aliye hai.

Mwanamke huyu aliteseka pamoja na kuteswa na mengi lakini kwa IMANI alipata kupokea Uponyaji baada ya kusikia Neno la Yesu Kristo lenye nguvu ya Kuponya. Hivyo kwa imani Wagonjwa wataponywa na kupata afya tena.

Wakati mwanamke yule anashika pindo la vazi la Yesu Kristo, nguvu zilizomtoka Yesu Kristo, ndizo zilizokwenda kufanya uponyaji kwa mwanamke huyu kwa Imani, hivyo ni dhahiri pasipo Imani hakuna nguvu ya Mungu kuingia na kuponya. Unaweza kuguswa na Watu au Watumishi wa Mungu na usipone lakini ukiamini kabisa na usione shaka moyoni mwako hapo ndipo utakapo pokea.“Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kkwa kinywa hukiri hata kupata wokovu.”  Warumi 10:9-10

Imani yetu katika Yesu Kristo Yesu sharti ivuke mipaka iliyowekwa mbele yetu, maana kwa Imani BWANA anasema,
“Nitakwenda mbele yako, na kupasawazisha mahali palipoparuza, nitavunja vipande vipande milango ya shaba, na kukata-kata mapingo ya chuma.” Isaya 45:2

WATU WANAWEZA KUKUCHEKA KWASABABU YA IMANI YAKO KATIKA MUNGU, usiogope vicheko vyao bali kaza roho kwa Imani maana lipo Jibu kwa kuwa Mungu hufungua njia mahali pasipo kuwa na njia. Angalia mfano huu wa ufunguo wa imani; “

 “Hata alipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu? Lakini Yesu, aliposikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu. Wala hakumruhusu mtu afuatane naye, ila Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye Yakobo. Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia, akawaambia, mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu. Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, wakamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwambo yule kijana. Akamshika mkono kijana, akamwambia, Talitha, kumi, tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka. Mara akasimama yule kijana, akaenda; maana alikuwa amepata umri wa miaka kumi na miwili. Mara wakashangaa mshangao mkuu. Akawaonya sana, mtu asijue habari ile, akaamuru apewe chakula.” Marko 5:35-43

Katika msiba Yesu anaangalia imani ya yule mkuu wa Sinagogi ili apate kutenda muujiza. Kwa maana Imani ahitaji ushabiki wa watu bali Imani inahitaji mtu mwenye kujua Neno la Mungu na kuliamini. Watu walimcheka Yesu Kristo pale aliposema mtoto hajafa bali amelala, Yesu akamwamsha, akamwambia kijana amka naye akawa mzima. Vivyo hivyo inawezekana upo kwenye ndoa miaka mingi hujapata mtoto, Kwa Imani tumbo lako lifunguliwe milango yake na upate watoto wa kiume na wakike.

 “Kwa Imani hata Sara mwenyewe alipokea uwezo wa kuwa na mimba, alipokuwa amepita wakati wake; kwa kuwa alimhesabu yeye aliyeahidi kuwa mwaminifu.” Waebrania 11:11

SARA alipoambiwa atabeba mimba na kuzaa aliona ni kichekesho kwake maana alikuwa mzee. Hali halisi ya mwili wa Sara ilimfanya apoteze imani ya kuzaa. Wako watu wengi wa Mungu wanaopishana na Baraka zao toka kwa BWANA kwa sababu ya kuhesabu miaka ya mapito yao na kuona Mungu amechelewa na kinachozaliwa ni kukata tamaa kwa mfano wa Sara. “Basi Ibrahimu na Sara walikuwa wazee, na umri wao mkubwa, na Sara alikuwa amekoma katika desturi ya wanawake. Kwa hiyo Sara akacheka moyoni mwake, akisema, Niwapo mkongwe, nitapata furaha, na bwana wangu mzee? BWANA akamwambia Ibrahimu, mbona Sara amecheka akisema, Mimi kweli nitazaa mwana, nami ni mzee? Kuna neno gani lililo gumu la kumshinda BWANA? Kwa muhula wake nitakurudia, wakati huu huu mwakani, na Sara atapata mwana wa kiume.” Mwanzo 18:11-14

Katika mambo yote Mungu hufanya kazi na wenye Imani ili apate kuwapatia Mema kwani ndio wale walioitwa kwa kusudi lake, Sisi tu watoto wa Mungu basi sasa tu warithi wa Baraka na Ustawi wa Kimungu, turithio kwa Imani pamoja na Kristo Yesu. Imani ni kutarajia yasiyowezekana kutarajiwa.

SARA alimpokea Isaka katika hali ya kutokutarajiwa kwani alikuwa mkongwe wa miaka mingi. Tangu Mungu atamke Ahadi ya uzao wa Sara, miaka ishirini na tano ilipita. “Nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani, na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa. Basi Abrahamu akenda kama BWANA alivyomwamuru, Lutu akaenda pamoja naye. Naye Abrahamu alikuwa mtu wa miaka sabini na mitano alipotoka Harani.” Mwanzo 12:3-4

IBRAHIMU alishakata tama juu ya ahadi ya Mungu ya kupata mtoto kupitia SARA, maana kimwili Sara alikuwa ni mzee asingeweza tena kuzaa. (biologically)
“Mungu akamwambia Ibrahimu, Sarai mkeo, hutamwita jina lake Sarai, kwa kuwa jina lake litakuwa Sara. Nami nitambariki, na tena nitakupa mwana kwake, naam, nitambariki, naye atakuwa mama wa mataifa, na wafalme za kabila za watu watatoka kwake. Ndipo Ibrahimu akaanguka kifudifudi akacheka, akasema moyoni, je! Mtu wa umri wa miaka mia, kwake atazaliwa mtoto? Naye Sara mwenye umri wa miaka tisini atazaa? Ibrahimu akamwambia Mungu, Lau kwamba Ishmaeli angeishi mbele yako.”  Mwanzo 17:15-18

·        Kwa imani kila mlango uliofungwa utafunguliwa, hatuhitaji kuangalia historia uliyopitia au hali ya mwili wako bali unachopaswa kuangalia ni Uweza na Nguvu za Mungu aliye
hai ambaye yeye hashindwi na jambo lolote.

 “…lakini mwenye haki ataishi kwa imani yake.” Habakuki 2:4

“BWANA ametukumbuka, naye atatubariki sisi. Ataubariki mlango wa Israeli, Ataubariki mlango wa Haruni, Atawabariki wamchao BWANA, wadogo kwa wakubwa.” Zaburi 115:12-13

Ushindi wetu katika ulimwengu wa Roho na mwili hutegemea Ufunguo wa Imani.


Itaendelea.....

Wednesday, November 23, 2016

MWENENDO WAKATI WA UCHUMBA

Mambo ya kufanya na yasiyofaa kufanya kabla na wakati wa uchumba

Mhandisi Lucas & Happiness Mgalula (TAG City Harvest Church)


Kila mtengenezaji huweka kitabu cha maelekezo ili kuelezea namna ya utumizi wa kitu husika.

Mungu ametupa nguvu na twaenda kwake kujifunza kuhusu udhibiti wa nguvu hizo, Power & Control

Mara nyingi huwa tunaangalia uchumba lakini kuna mahali umeanzia, mahusiano ya urafiki. Tunaangalia namna vijana waliookoka wanavyopaswa kuenenda katika mahusiano kuelekea ndoa.

Umri huu ni kipindi muhimu ambacho hakirudi tena, ni cha muhimu kwako, kwa familia, wazazi, kanisa, jamii nzima na Mungu. Wote wanakutegemea upite salama na kufanikisha kusudi la Mungu.

Kabla ya Uchumba

Kipindi unachojiuliza ikiwa utapata mtu sahihi na ikiwa moyo wako utamkubali. Hata usipoijua njia, hautapotea

I.      Mahusiano na wenzako

-  Fanya ni utaratibu wako kuomba juu ya mahusiano uliyonayo na wenzako ili ule utakaopelekea ndoa ushamiri zaidi na yale yatakayoleta vurugu yafe! Mwanzo 24:12-14 aliyetumwa kumtafutia Yakobo mke alikuwa makini kuomba hivyo
-  Mwambie Mungu akusaidie ili ule uhusiano ulio makini uuone.
-  Anaweza kutokuwa na vigezo vyote unavyovidhania lakini akawa ndiye hasa. Isaya 30:21 Hii ndiyo njia, ifuate

II.  Tafuta ushauri wa wenye hekima wa Mungu

-  Unapoona kama uhusiano mmoja unashamiri na unaweza kupelekea kwenye uchumba, tafuta ushauri wa wenye hekima waliookoka hasa wanandoa.
-  Kuna mambo mengi njiani ambayo utahitaji maombi na msaada wao.
-  Mungu hukupa mwanamke/mwanaume, kazi kwako kumjenga awe mke/mume
-  Hakuna anayekuwa amekamilika, maana hakuna aliyekuwa mume au mke kabla hamjatangazwa hivyo na kuanza kuishi pamoja. Hakuna anayenunuliwa sokoni akiwa kamili
-  Hekima huja kwa kusikia au kupitia, hakuna aliyekuwa amepitia ndoa kabla, hivyo ni vema kupata wanandoa wenye hekima wakusaidie
-  Usiufiche uhusiano wako unaoelekea kwenye uchumba, ni hatari

III.    Kuwachukulia wote kuwa ndugu zako

-  Watu wote unaohusiana nao kanisani na kwingineko, wachukulie kama dada au kaka. Mvulana usiwadharau wadada na msichana usiwachukulie wakaka kama watu waonevu
-  Kuna aina hii ya heshima ambayo kaka na dada wanakuwa nayo kwa kila mmoja. 1Timotheo 5:1-2 Kwa usafi wote, nia, kimawazo, maneno na matendo
-  Sote tu wa damu moja, tumenunuliwa kwa damu ya Kristo
-  Kwa kuhusika katika shughuli nyingi za kanisa zinazoweza kuwaleta pamoja na mkafahamiana, ndipo waweza kujua namna ya kuamua ikiwa tabia zenu zitaendana na mtachukuliana. "Birds of feathers flock together"
-  Baada ya kumfahamu, heshima iendelee, hapa ni kabla ya kuwa “Mr. Special” au “Ms. Special”
-  1Wakorintho 13:4-8 (Sifa za Upendo)
-  Linda moyo wako kuliko vyote ulindavyo, maana ndiko zitokako chemchemi za uzima
-  Kama kuna kitu "special" baina yenu ni bora ukiseme na siyo kuficha ficha. Acheni kung'ang'aniana kama kumbikumbi kila uendako naye yupo halafu mnasema hakuna kinachoendelea baina yenu. Hiyo ni mbaya na hatari na unaweza kukosa "opportunity" na hata kumkosea Mungu.

NOTE: Don't treat anyone special! Don't single her out! Avoid over-clinging to one person when there is nothing-marital material!

Kabla ya Ndoa

-  Usimtembelee mtu wa jinsia tofauti (mchumba) kwake mkiwa peke yenu.
-  Usimfulie, kumpikia au kumsafishia nyumba. Kwa nini upate privileges za ndoa kabla? Una haraka gani?
-  Inaweza kuanza vizuri na kwa nia njema lakini mkaangukia kwenye "premarital sex and pregnancies" ambayo italeta majuto, uchungu na chuki

Wakati wa mahusiano/uchumba

-  Usichochee mapenzi kabla ya wakati wake. Ni mchumba wako lakini haimaanishi unao uhuru wa kufanya lolote utakalo. Huwezi kuwa Rais kabla ya kuapishwa
-  Mwili wako unatambua tayari kwamba huyu ni mtu maalumu, nao unajiandaa na kuitikia hivyo. Kuwa makini.
-  Avoid physical touches, as they will result into premarital sex and unplanned pregnancies
-  Uchumba unaweza kuvunjika. Mungu atakupa amani ndani yako kuendelea mbele, isiwe mzigo kwako ukatumia nguvu nyingi kumridhisha au kumweka kwako halafu mwitikio ukiwa mdogo unaanza kujiuliza kwa nini. Usijilazimishe au kukubali kwa kumhurumia. Ikiwa haiwezekani sema kwa upendo na upole. Ikiwa ana shida, ndiyo maana Mungu akakufunulia wewe ili uchukue hatua za Kikristo kumsaidia

Swali: Vipi kuhusu kutoa zawadi kwa mtu uliye kwenye mahusiano naye/mchumba?
-  Zawadi inaweza kuwa aina fulani ya rushwa, inaufunga moyo wa mtu. Anaweza kukukubali kwa hizo kwa kuwa umeuteka moyo wake na utalazimika kuwa unafanya vitu kwa ajili yake ili aendelee kukukubali

-  Ni bora ukilazimika au kujisikia kutoa zawadi, utoe ambayo haitaumiza moyo wako mambo yakienda kombo. Usianze kununua naye vitu vya thamani, kuwekeza pamoja, kujenga, viwanja na kadhalika.


-  Ni vema upendo ukaja kawaida, zawadi zitafuata kwa nafasi yake

Tuesday, November 22, 2016

MSANII WA WIKI - RITHA KOMBA


RITHA KOMBA KATIKA MSANII WA WIKI
Ritha Komba 
Ni wiki nyingine tena tunakutana katika “Msanii wa Wiki” na leo tuko na Mwimbaji mwingine wa nyimbo za Injili anayechipukia, si mwingine bali ni Ritha Komba

Kuna mengi usiyoyajua kumhusu, lakini leo nafasi ni yako kufahamu angalau machache zaidi kumhusu yeye. Tujumuike pamoja katika safari hii fupi ya kufahamu Ritha Komba, msanii wetu wa wiki hii

Rejoice Blog: Je, umeokoka? Wapi unaabudu?

Ritha: Nimeokoka, naabudu katika Kanisa la  Kiinjili la  Kilutheri

Rejoice Blog: Historia yako kwa kifupi ya kuimba, yaani ulianzaje na wapi ulianzia?

Ritha Komba
Ritha: Mimi nilianza kuimba mwaka Jana pale mtumishi wa  Mungu aliponiambia nianzishe pambio kanisani. jumapili iliyofuata nilienda nyumbani nikasema sijawahi kuanzisha pambio wala kuimba kanisani, je  itakuwaje? Nikasema hapana, sitaimba wimbo wa mtu, natunga mwenyewe. Nikatunga wimbo mfupi tu na siku ilipowadia nilipoitwa kuimba nikaimba wimbo wangu binafsi na ukapendwa. Tokea hapo nikawa napewa nafasi ya kuimba na mpaka hivi sasa nimekua muimbaji

Rejoice Blog: Katika kuimba kwako, je, umeshatoa albamu yoyote? Jina ya albamu?

Ritha: Nimeshatoa  album audio na video, nasubiri kuizindua tarehe 18 Disemba pale Shalom Eloi Center, Kigamboni Kisiwani ndipo nianze kuisambaza

Rejoice Blog: Albamu yako inaitwaje?

Ritha: Albamu yangu inaitwa 'Mungu wa  Ajabu' na video hii inapatikana YouTube

Rejoice Blog: Wimbo unaoupenda zaidi kati ya nyimbo zako ni upi?

Ritha: Katika album yangu napenda nyimbo zote, ila unaonibariki sana ni  wimbo wa  Usifiwe

Ritha Komba
Rejoice Blog: Ni kwa sababu gani unaupenda wimbo huo zaidi?

Ritha: Ni  wimbo ambao unagusa moyo wangu sana kwa matendo ambayo Mungu ameyatenda kwangu pasipo mimi kutenda jema  lolote

Rejoice Blog: Nani anasambaza na kusimamia kazi zako?

Ritha: Mpaka sasa bado sijapata msambazaji, nipo kwenye mchakato huo wa kutafuta msambazaji wa kazi zangu

Rejoice Blog: Ni msanii gani wa muziki wa Injili anayekuvutia zaidi na unapenda kufuatilia kazi zake?

Ritha: Navutiwa sana na waimbaji wengi wa  Nyimbo za Injili; naweza kusema Angel Bernard, Jessica Honore BM na Beatrice Mwaipaja. Huwa napenda sana kufuatilia kazi za hawa waimbaji

Rejoice Blog: Kuna mafanikio yoyote umeyapata katika uimbaji wako?

Ritha: Mafanikio niliyoyapata ni kuwa msomaji mzuri wa  Neno la  Mungu na kujikuta nakuwa mwenye upendo, furaha na amani. Lakini pia najuana na watu wengi zaidi tofauti na hapo awali

Ritha Komba
Rejoice Blog: Umekutana na changamoto gani katika huduma yako ya uimbaji?

Ritha: Changamoto ni  nyingi hasa  kwa sisi ambao tunachipukia, vitu vingi tunakua hatuvifahamu. Lakini pia suala la  uchumi ni  changamoto kubwa sana, kurekodi kunahitaji hela, kutengeneza video nako kunahitaji hela, matangazo ili kazi iwafikie wengi pia inahitajika hela. Hizo ni  changamoto kubwa nilizoziona

Rejoice Blog: Unaonaje muziki wa Injili hapa Tanzania?

Ritha: Muziki wa Injili umekua kwa kasi kikubwa sana, sio kama ule wa zama hizo; mambo yamebadilika. Umekuwa ni  muziki wenye ushindani mkubwa. Kwa hiyo hapo ni  kujitoa kwa dhati kuifanya kazi ya Bwana bila kukata tamaa

Rejoice Blog: Unatoa ujumbe gani kwa waimbaji wa nyimbo za Injili ambao kwa njia moja ama nyingine wanajisahau na kujichanganya na mambo ya dunia hii?

Ritha: Wito  ninaotoa mimi ni  huu; kama tumejitoa kwa nia ya dhati kuifanya kazi  ya Mungu kupitia uimbaji na iwe  hivyo, tusitengeneze makwazo kwa Muumba wetu

Ritha Komba
Rejoice Blog: Zaidi ya kuimba ni kitu gani kingine unakifanya?

Ritha: Mimi ni  mjasiriamali, nasomea journalism and media

Rejoice Blog: Je, kimaisha uko wapi? Ndoa na watoto vipi?

Ritha: Nimeolewa sina mtoto bado

Rejoice Blog: Una ujumbe gani kwa Waimbaji wa Nyimbo za Injili hapa Tanzania?

Ritha: Ujumbe kwa waimbaji wenzangu, tufanye kazi  ya Mungu kwa moyo na tupendane sisi kwa sisi bila kujali nani  anaimba vizuri, nani haimbi vizuri. Tuinuane maana kwa Mungu hakutaangaliwa sauti yako ilikuaje au umaarufu, bali Mungu ataangalia tulijitoaje katika kumtumikia yeye

Rejoice Blog: Kwa jamii inayoguswa na kuburudishwa na nyimbo za Injili una ujumbe gani kwao?

Ritha Komba
Ritha: Napenda kuiambia jamii kuwa; Neno la  Mungu huwa halipunguzwi wala kuongezwa. Wasikilize nyimbo zote za waimbaji bila kubagua ili wapate ujumbe  mzuri. Wajiandae kupokea nyimbo zangu zitawabariki, kuwafariji na kuwasogeza karibu zaidi na Mungu

Rejoice Blog: Ahsante sana Ritha kwa muda wako, Mungu akubariki na kukuinua unavyoendelea kumtumikia kwa uaminifu

Ritha: Ameen!



Unaweza kuendelea kumfuatilia Ritha Komba katika mitandao mbalimbali ya kijamii ikiwemo Facebook, Instagram, YouTube na Twitter

Unaweza pia kuwasiliana naye kwa simu  namba 0712496727


~~~ Huyo ndiye Ritha Komba, usikose wiki ijayo tena, tunakutana kumfahamu zaidi msanii mwingine. Ubarikiwe! ~~~