Tuesday, August 26, 2014

Kuna Uhusiano Mkubwa kati ya Usalama na Ubora wa Nafsi yako na Uhai wa Kanisa -III na Mwalimu Samwel Mkumbo

 

 Mwalimu Samuel Mkumbo pichani
Karibu atika mifululizo yote ya somo hili kutoka mwanzo mpaka sasa imekuwa ni suala la kuangalia ni kwa jinsi gani nafsi zetu zinahusika sana katika Uhai wa Kanisa. Sehemu ya mwisho nitasema nawe kwa kifupi sana kuhusu Uhusiano wa nafsi ya Kanisa.

Karibu tujifunze pamoja…..

Luka 12:15 inasema hivi;

Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.

Ni heri kila mmoja akahakikisha ya kwamba Nafsi yake iko na furaha kila wakati, kwa ajili ya uhai wa kanisa lako, lakini pia kwa ajili ya uhai wa nyumba yako kama msingi wa kanisa, kwa ajili ya ofisi yako, kwa ajili ya ukoo wako.

Lakini pia ni vema kila mmoja akahakikisha anafanya bidii kumfurahisha mwingine na kuifanya nafsi ya mwingine isiwe na jeraha hata moja, kuifanya nafsi ya mwingine isitende dhambi, kila mmoja acheze karibu na mwenzake, kama kucheza basi tucheze peke yetu, hakikisha unamlinda mwenzake asipate shida wala asipotee.

1 Wakorintho 8:12 tunasoma hivi;

Hivyo, mkiwatenda dhambi ndugu zenu na kuitia jeraha dhamiri iliyo dhaifu, mnamtenda dhambi Kristo

Kuna Uhusiano Mkubwa kati ya Usalama na

Ubora wa Nafsi yako na Uhai wa Kanisa

Sasa labda tutazame kwa nafasi nyingine uhusiano wa Nafsi yako ikiwa na Usalama na ubora wa nafsi yako na Uhai wa Kanisa ikiwa ni la nyumbani au ni mahali unapoabudu au ofisini kwako au hata shuleni kwako unakosoma.

Labda niweke jambo hili la msingi, tunapozungumzia kanisa ni lazima tukajua ya kwamba si suala la dhehebu moja tu au suala la watu wanaosali kwa pamoja lakini suala la Kanisa ni jambo linalohusu watu wote waliookoka na wanaomkubali BWANA YESU kuwa ni mwokozi wa maisha yao na Mfalme wa Ulimwengu wote.

Sasa kuna shida ambayo ni muhimu tukaishughulikia vizuri kidogo ili tusipate shida tunapoangalia utekelezaji wa Somo hili, na jambo lenyewe ni lazima akili zetu na fahamu zetu zifunguke tukajua mambo kadhaa ili tuone Umuhimu wa kuona Nafsi ya kila mmoja inakuwa salama na bora ili Kanisa liweze kuwa Hai.

1 Wakorintho 3:16-17 tunasoma hivi;

Hamjui ya kuwa ninyi mmekuwa hekalu la Mungu, na ya kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu? Kama mtu akiliharibu hekalu la Mungu, Mungu atamharibu mtu huyo. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, ambalo ndilo ninyi.

Sasa kuna jambo la msingi hapo natamani tulitazame kwa makini sana sana, maana kama tusipolitazama kwa makini tunaweza tusielewe vizuri, na hilo jambo linatuonesha Uhusiano uliopo kati ya Usalama na Ubora wa Nafsi yako inavyohusiana na Uhai wa Kanisa la Tanzania, Kanisa la Ulimwengu mzima lakini pia kuanzia na Kanisa la Nyumbani kwako na mahali unapoabudu.

Basi tuutazame huo mstari kwa makini sana sana, kuna maneno kadhaa ya huo mstari natamani tuyatazame kwa makini …..Hamjui ya kuwa NINYI mmekuwa hekalu la Mungu….. na ya kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani YENU?....... Kama MTU akiliharibu hekalu la Mungu,… Mungu atamharibu MTU huyo….. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, ambalo ndilo NINYI.

Maneno niliyoyaweka kwa herufi kubwa yana maana kubwa sana, Paulo kwa uwezo wa Roho Mtakatifu anawaandikia Wakorintho akitaka kuwaonesha ni jinsi gani Uhusiano wa Kanisa unavyotengenezwa na unavyotegemea mtu mmoja mmoja. Anapozungumzia Hekalu la Mungu anasema ni NINYI au ndilo SISI kama tukijiweka kwenye nafasi ya Wakorintho na ambayo ni nafasi muhimu lazima tujiweke hapo ili hiyo nafasi tuichukue kwa Umuhimu mkubwa sana.

Jambo amabalo ni la kulitazama kwa makini kwenye mistari hiyo ni kwamba inapozungumziwa kanisa basi tunatazama kama Muunganiko wa watu,. Maana HEKALU LA MUNGU (moja) linajengwa na NINYI (wengi), lakini pia inawezekana hilo Hekalu la Mungu ambalo ni watu wengi likaharibiwa na MTU yaani mmoja. Sasa basi kuna jambo la kulitazama tena hapo kwa makini Zaidi, kwamba kama Hekalu la Mungu linalojengwa na SISI linaweza kuharibu na YULE au WEWE basi pia linaweza kujengwa na WEWE- Nitalielezea hilo baadae kwa undani.



1Wakorintho 6:19 tunasoma hivi;

Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe;

Nataka tutazame vizuri maneno mengine kwenye mstari huo ambayo hayatofautiani sana maneno yaliyoelezwa kwenye mistari ile tuliyotangulia kuitazama hapo juu (1Wakorintho 3:16-17), maana katika mstari huo hapo anaeleza wingi wa waliookoka kama mtu mmoja na ambaye huyo mtu mmoja anatengeneza Hekalu la Mungu, lakini cha ajabu Paulo anaandika kwa wengi kana kwamba kwa mtu mmoja.

Tazama kwa makini maneno haya;

Au HAMJUI ya kuwa MWILI WENU ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani YENU, MLIYEPEWA na Mungu? Wala NINYI si mali YENU wenyewe;

Anasema hivi

Au HAMJUI (wengi) ya kuwa MWILI WENU (mmoja) ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani YENU MLIYEPEWA (wengi) na Mungu? Wala NINYI si mali YENU wenyewe;

Katika yote nataka nikuoneshe ya kwamba haijalishi kwa Ukubwa wake au kwa udogo wake, kwa umaarufu wake au kwa kutokujulikana kwake, KANISA linaanza na Nafsi moja moja na haijalishi kwa wingi wake waliopo humo ndaniau idadi ya waliookoka katika mji Fulani au nchi Fulani bado kanisa litahesabika kama MTU MMOJA au MWILI MMOJA.

Mpaka hapo tujaribu kurudi kidogo kwenye ule mstari wa 1Wakorintho 3:17 unasema hivi;

Kama mtu akiliharibu hekalu la Mungu, Mungu atamharibu mtu huyo. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, ambalo ndilo ninyi.

Nataka tuone madhara yanayoweza kutokea mtu anapojaribu kuliharibu Hekalu la Mungu yaani Kanisa ambalo ni Ninyi mlio wengi mnaotengeneza Mtu au Kitu kimoja katika kumtukuza Kristo au kusimamisha Ufalme wa Mungu. Maandiko yanasema mtu akiliharibu Hekalu MUNGU atamharibu mtu huyo.

Sasa tuondoe mawazo ya kuwafikiria watu kama wakina Sauli ambao wanaliharibu Hekalu au Kanisa kwa sababu Hawajaokoka, au tusiwafikirie Wakuu wa makuhani wanaokataza watu wasiseme tena wala kupoza Wagonjwa kwa Jina la YESU, tukiangalia hivyo tutakosa maana ya msingi sana sana, hebu tuutazame huo mstari kama unawaambia watu au unamuonya Mtu anayeliharibu Kanisa huku naye ameokoka au yumo ndani ya Kanisa.

Na kulingana na maandiko inawezekana kabisa mtu akaliharibu Kanisa wakati mwenyewe yumo humo ndani yake, haijalishi anajua kama analiharibu Kanisa au la, lakini kuna uwezekano kabisa akawa analiharibu kanisa wakati na yeye yumo ndani yake.

Matendo 20:28-30 tunasoma hivi;

Jitunzeni nafsi zenu, na lile kundi lote nalo, ambalo Roho Mtakatifu amewaweka ninyi kuwa waangalizi ndani yake, mpate kulilisha kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe. Najua mimi ya kuwa baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wakali wataingia kwenu, wasilihurumie kundi; tena katika ninyi wenyewe watainuka watu wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.

Sasa kuanzia mstari wa 30 inaonesha kabisa ya kwamba si kwamba mharibu anaweza kutoka nje ya kundi lakini kumbe anaweza kutoka ndani ya kundi, hata kama ataonekana ni kama mtu anayekata tawi alilokalia mwenyewe lakini hiyo si kitu lakini ndio anaharibu sasa. Na MUNGU hawezi kukaa kimya anapomuona mtu anaharibu au

anapoleta au kuingiza kitu kinachoharibu kanisa hata kama huyo mtu hajui lakini MUNGU hatamuacha, lazima atampa adhabu Kulingana na ule mstari wa 1Wakorintho 3:17.

Lakini nataka niweke jambo Fulani ndani yako ya kwamba, kama mtu alikuwa mpo naye pamoja kasha akaanza kutenda mambo tofauti na kuliharibu kundi lazima mtapata shida, lakini pia MUNGU akimhadhibu mtu huyo bado kwa watu wenye Uchungu na Kanisa watapata shida lazima maana wanajua Umuhimu wake, hivyo hawatafurahia adhabu ya MUNGU aliyoipata, hivyo basi Nafsi moja ikiharibika lazima kuna jambo linabadilika kwenye Kanisa.

Matendo 5:5-11 inasema hivi;

Anania aliposikia maneno haya akaanguka, akafa. Hofu nyingi ikawapata watu wote walioyasikia haya. Vijana wakaondoka, wakamtia katika sanda, wakamchukua nje, wakamzika. Hata muda wa saa tatu baadaye mkewe akaingia, naye hana habari ya hayo yaliyotokea. Petro akamjibu, Niambie, Mlikiuza kiwanja kwa thamani hiyo? Akasema, Ndiyo, kwa thamani hiyo. Petro akamwambia, Imekuwaje hata mkapatana kumjaribu Roho wa Bwana? Angalia, miguu yao waliomzika mumeo ipo mlangoni, nao watakuchukua nje wewe nawe. Mara akaanguka miguuni pake akafa; wale vijana wakaingia wakamkuta amekufa, wakamchukua nje, wakamzika pamoja na mumewe. Hofu nyingi ikawapata kanisa lote na watu wote walioyasikia haya.

katika mistari hiyo natamani nikuoneshe kilichotokea kwa Anania na Safira na Uhusiano na Kanisa, sasa ninawinda mstari ule wa 11 ambao unatuonesha jambo Fulani lililotokea kwenye Kanisa na jambo lenyewe ni HOFU iliyo ZIMISHA nafsi zao kwa ndani, sio hofu tu ya kusema MUNGU ni MKUU lakini pia inakuwaje mtu akiwa na shida ya kuonana na Petro au mtume Fulani, na ndio maana hawakuwa na Ujasiri wa kusema jambo lolote na waliona ni heri kutenda dhambi ya kunung’unikakuliko kuonana na Mitume na kuwaambia shida zao.

Yote hiyo inatokana na nafsi ya mtu mmoja Anania ilipoharibika ilikuwa haiku Salama iliyomshauri Mkewe Safira na wote wakatenda jambo lililoharibu Kanisa kwa namna moja au nyingine, na halikuharibu kanisa kwa mtindo ambao watu waliondoka, la hasha! Watu walikuwepo na walizidi kuongezeka katika kanisa (MATENDO 4:14) lakini ndani yake kuna WOGA/HOFU ambayo ilisababisha watu wawaogope mitume kuwaeleza shida zao wakaona ni vema tu wakanung’unika (MATENDO 6:1)

Nataka niseme ya kwamba suala si tu kuona watu, lakini Nafsi ya kila mmoja inatakiwa iwe Salama, maana nafsi Fulani ikiharibika basi ujue hakuna Usalama hapo, na ujue kabisa kunahitajika kuhakikisha kila nafsi ndani ya Kanisa iko Salama na iko Bora.

Waebrania 12:15 tunasoma;

Mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.

Nimeweka huo mstari hapo ili tutazame jambo hilo kwa mtazamo wa Upande wa pili ya kwamba kama mtu mmoja akipungukiwa na Neema ya Mungu anaweza kuleta shina la Uchungu ambalo linawakwaza wengi, Je ikatokea mtu mmoja akaongezewa Neema ya Mungu nini kitatokea?

NADHANI SHINA JEMA SHINA LA UTAMU, SHINA LA FURAHA, SHINA LA KICHEKO, SHINA LA WEMA LINACHIPUKA NA KUWABARIKI WENGI.

Aaaaameen!!!

Umebarikiwa.

NURU Ministry:

mkumbosj@gmail.com

www.facebook.com/mwlsamwelmkumbo

+255 753 – 204 743

No comments:

Post a Comment